Tuesday, August 23, 2016



MKUU WA WILAYA YA CHEMBA AFANYA ZIARA KATIKA TARAFA YA FARKWA NA KWAMTORO.

Mkuu wa Wilaya ya Chemba Ndugu Simon Odunga alifanya ziara katika Tarafa ya Farkwa na Kwamtoro kuanzia tarehe 19-20/8/2016 akiambatana na Kamati ya ulinzi na Usalama ya Wilaya na baadhi ya watendaji wa Halmashauri.
Katika ziara hiyo alifanya mikutano ya hadhara na wananchi wa vijiji vya Tumbakose, Farkwa, Bubutole, Gonga, Kwamtoro, Magungu na Sanzawa. Alizungumza na wananchi kuhusu masuala ya Elimu, Maji, Afya, Ulinzi na Usalama, Chakula, Ardhi, na kusikiliza kero na changamoto za wananchi wa maeneo hayo.

Katika kijiji cha Tumbakose wananchi walikuwa wanavutana juu ya ujenzi wa ofisi za kata katika kijiji cha Tumbakose au Humekwa. Mkuu wa Wilaya aliwashirikisha wananchi kwa kuwaomba waseme ni kijiji gani wanataka kiwe kata.Wananchi  walisema  kijiji cha Tumbakose ndiyo maamuzi yao ya kwanza kuwa kata na waliamua wakiwa katika kata mama ya Gwandi kabla ya kugawanywa. Kutokana na uamuzi huo, Mkuu wa wilaya alitoa agizo kwa viongozi wa vijiji vya Humekwa, Hawelo na Tumbakose kuanza ujenzi mara moja ya ofisi za kata katika kijiji cha Tumbakose. 

Mkuu wa Wilaya akiwa katika Mikutano ya hadhara alikemea tabia ya wanaume kufanya mapenzi na wanafunzi wa shule kwani ni kosa la jinai. Alitoa agizo kwa vyombo vya dola kuwakamata wale wote wanaojihusisha na tabia hiyo mbaya ili sheria iweze kuchukue mkondo wake. Alisema kuna tabia ya wazazi wa wanafunzi wanaopewa mimba na wahalifu kurubuniwa kwa kupewa fedha ili wazazi hao wasiende kutoa ushahidi mahakamani. Alisisitiza wazazi wanao fanya hivyo waache mara moja kwani nao ni wahalifu watakamatwa na kufikishwa mahakani. Pia alipata fursa ya kuwasilimia wanafunzi wa sekondari ya Farkwa na kuwasihi kusoma kwa bidii kwani elimu ndiyo dira ya maisha na waepuke migomo ambayo mwisho wako ni kufukuzwa shule. Aliwahidi wanafunzi kuwa serikali ya wilaya itanunua pampu mpya ya maji na kuifunga wiki ijayo ili kuondoa tatizo la maji wanalopata kwa sasa.

 Mkuu wa wilaya aliagiza vijiji vyote vya wilaya ya Chemba kuunda kamati za maji za vijiji pia vikishirikisha wanawake kama Sera ya maji inavyoagiza. Kamati hizi zitaratibu uendeshaji wa maji katika vijiji vyao na fedha inayopatikana itatumika kuboresha matandao wa maji hapo kijijini kwa kununua vifaa.

Mkuu wa wilaya aliagiza ifikapo mwezi wa 10/2016 kila kaya katika vijiji vyote vya wilaya ya Chemba kuwa na choo na pia kujiunga na mfuko wa afya ya jamii (CHF). Aliwataka watendaji wa vijiji na kata kusimamia zoezi hilo kwani baada ya muda huo kupita atafanya ziara ya kukagua kama wametekeleza. Amesisitiza gharama za kulipia mfuko wa afya ya jamii kwa watu sita katika kaya ni Tsh.13,000/= na watapata huduma ya afya katika zahanati, kituo cha afya na hospitali bila kutoa gharama yeyote tena kwa mwaka mzima. Aliongeza kwa kusema wazee wote wenye umri wa kuanzia miaka 60 na kuendelea hasa wasiojiweza wanatakiwa kupatiwa vitambulisho ili watibiwe bure kama ilivyo kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka 5. Alitoa onyo kwa wahudumu wa afya walio na tabia ya kutotoa huduma kwa haraka kwa wanachama wa mfuko wa CHF na kupendelea wanao toa fedha mkononi waache tabia hiyo mara moja kwani sheria za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yao ikiwa ni pamoja na kusimamishwa kazi ili wakafanye kazi zingine wanazoona zinafaa kuliko kuwanyanyasa wananchi.

Mkuu wa wilaya alisema, kuna baadhi ya wananchi, viongozi wa vijiji na kata wanawakaribisha wahamiaji katika vijiji vyao na kusababisha migogoro ya ardhi. Kuanzia tarehe 06/8/2016 amesimamisha uuzwaji wa ardhi na ukaribishaji wa wahamiaji katika wilaya ya Chemba hadi hapo atakapo toa maelekezo mengine. Ameagiza viongozi wote wa vijiji, kata, tarafa na wilaya kusimamia zoezi la kupanga matumizi sahihi ya ardhi kwa kutenga maeneo ya wafugaji na wakulima ili kuepuka migogoro ya wakulima na wafugaji.
Pia alionya wale wote wanao leta choko choko za uvunjifu wa amani kwa kusema watashiriki maandamano ya UKUTA yanayoandaliwa na chama cha chadema kuanzia tarehe 01/9/2016 wasithubutu kufanya hivo kwani watakabiliana na vyombo vya dola na hawataonewa huruma kwa sababu ni wavunjaji wa amani katika nchi yetu. Vilevile aliwasihi wananchi kuuheshimu Mwenge wa Uhuru kwasababu ni alama ya Uhuru wetu tuliopta mwaka 1961 ambapo mwasisi wa taifa letu Mwalimu J.K.Nyerere alipigania wakati anadai Uhuru na kuupandisha kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro. Akasisitiza kuwa bendera ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina alama ya Mwenge wa Uhuru, majeshi ya ulinzi na usalama kwenye kofia zao zina alama ya Mwenge wa Uhuru pia.

Kwa upande mwingine, Mkuu wa wilaya amesema Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dr. John Pombe Magufuli haitatoa chakula bure kwa mwananchi yeyote asiyefanya kazi. Amesisitiza kwa kusema  chakula kitatolewa kwa mwananchi ambaye amefanya kazi lakini kutokana na sababu za kidharura hakuweza kupata chakula kwa mfano, amelima lakini kutokana na ukame hakuweza kuvuna, amelima lakini wakati wa mavuno chakula kikaharibika kutokana na mvua kubwa kunyesha kama ilivyotokea kwa baadhi ya wananchi wa wilaya ya chemba kupata ugonjwa wa SUMUKUVU lakini serikali imewapatia chakuala bure. 

Katika mikutano ya hadhara Katibu tawala wa wilaya Ndugu Nyakia Ally aliwaambia wananchi kuwa atatoa namba ya simu kwa watendaji wa vijijiji vyote vya wilaya ya Chemba ili wawape wananchi namba hiyo lengo wawe wanatuma ujumbe wa meseji tu kuripoti kero wanazokumbana nazo na ofisi ya Mkuu wa wilaya itakuwa inazishughulikia.

Zifuatazo ni baadhi ya picha za mikutano ya hadhara ;


 Mkuu wa wilaya ya Chemba Ndugu Simon Odunga akiongea na wanafunzi wa Farkwa Sekondari.


 Mkuu wa wilaya ya Chemba Ndugu Simon Odunga akiongea na wananchi wa kijiji cha Bubutole kata ya Farkwa.


Katibu Tawala wa wilaya ya Chemba Ndugu Nyakia Ally akiongea na wananchi wa kijiji cha Magungu kata ya Mpendo.




  Mkuu wa wilaya ya Chemba Ndugu Simon Odunga akiongea na wananchi wa kijiji cha Kwamtoro.








Thursday, August 18, 2016

UGAWAJI WA CHAKULA KILICHOTOLEWA NA SERIKALI KWA WANANCHI WA WILAYA YA CHEMBA WALIOATHIRIKA NA UGONJWA WA SUMUKUVU.

Mkurugenzi Mtendaji (W) ya Chemba Dr.Semistatus H. Mashimba amesema, mnamo tarehe 12.08.2016 Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ilipokea agizo kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu ikitaka kwenda NRFA Dodoma kupokea mahindi kiasi cha tani 60 (Gunia 684) kwa ajli ya kuwagawia wananchi walioathirika na tatizo la ugonjwa wa SUMUKUVU.
Kufuatia agizo hilo Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ilifanya taratibu za haraka kuweza kwenda kuchukua mahindi hayo.

Magunia 229 yalisambazwa kwa wananchi waliokusudiwa katika vijiji vya Mondo, Kinkima, Itolwa, Chemka, Mlongia, Soya, Chang’ombe, Mwailanje, Mwaikisabe, na Isusumya. Magunia yaliyobaki yamehifadhiwa katika vijiji vya Chemba, Kinkima na Chemka kama tahadhari ya chakula kwa wagonjwa wengine wanaoweza kujitokeza.

Mkurugenzi Mtendaji (W) amesema, zoezi la kugawa chakula kwa wananchi walioathirika na SUMUKUVU lilifanyika kwa kushirikisha Wataalam kutoka Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji(W), Maafisa Watendaji wa Kata na vijiji wa maeneo husika na kusimamiwa kikamilifu na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Chemba.

Pia tathmini inaendelea kufanyika katika maeneo ya jirani na walikotoka wagonjwa ili kuwabaini wananchi wengine ambao wanaweza  kuwa na akiba ya chakula ambacho kimeharibika ili kukiteketeza na kuwagawia chakula kingine.Pia Halmashauri inafanya ufuatiliaji wa karibu kujua iwapo kuna wagonjwa wapya wanaojitokeza katika maeneo hayo.

Mkurugenzi Mtendaji (W) amesema, Wananchi waliopokea msaada huo wamemuomba Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Ndugu Jordan M. Rugimbana kufikisha shukrani zao za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dr. John Pombe Magufuli kwa Serikali yake ya awamu ya tano kwa msaada wa chakula waliopata.

Zifuatazo ni baadhi ya picha za matukio ya ugawaji wa chakula hicho.






















Thursday, August 11, 2016

MAONESHO YA NANE NANE MWAKA 2016 KANDA YA KATI DODOMA.
Maonesho ya Nane Nane mwaka huu 2016 kanda ya kati yamefanyika viwanja vya Nzuguni Mkoani Dodoma kwa kushirikisha Mikoa ya Dodoma na Singida.
Maonesho hayo ya Wakulima na Wafugaji maarufu kama sherehe za Nane Nane yalianza tarehe 01-08/08/2016 sehemu mbalimbali nchini na kitaifa yalifanyika Mkoani Lindi.
Afisa kilimo (w) ndugu Funda alisema, Maonesho hayo kwa kanda ya kati yalikuwa ni mazuri na Wilaya ya Chemba ilishiriki kwa kiasi kikubwa kuanzia tarehe 01- 08/08/2016. Idara tatu zilishiriki kuwakilisha wilaya kwa kuonesha shughuli mbalimbali zikiwemo; vipando mbalimbali, bidhaa za mbegu zilizosindikwa, mifugo, huduma ya uzazi wa mpango, upimaji wa ukimwi n.k.
Afisa Kilimo (w) alisema, Wilaya ya Chemba imepata Mafanikio kwa kupata cheti cha Ushiriki pamoja na  Mfugaji wa ng’ombe Bw.Mohamedi Deketi alipata zawadi ya mfugaji bora wa ng’ombe (mtamba asiye na mimba). Pia katika maonesho hayo, Naibu Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira (Mh.Antony Mavunde, Mb) alitembelea mabanda ya wilaya ya Chemba na kuona shughuli mbalimbali za ufugaji, kilimo n.k.

Zifuatazo ni baadhi ya picha katika maonesho hayo:














Tuesday, August 2, 2016

ZOEZI LA UHAKIKI WA VYETI VYA TAALUMA NA UTAALAMU KWA WAFANYAKAZI WA HALMASHAURI YA WILAYA YA CHEMBA LIMEANZA  RASMI LEO TAREHE 02/08/2016 MAKAO MAKUU YA HALMASHAURI YA WILAYA.



 Afisa Raslimali watu wa wilaya  Bi Carolina Kayombo akihakiki vyeti vya watumishi.

 Afisa Elimu vifaa na takwimu (M) wa wilaya akihakiki vyeti vya watumishi.


 Watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Chemba wakiwa kwenye uhakiki wa vyeti




 Afisa Elimu wilaya (M) Bi.Dafroza Ndalichako akihakiki vyeti vya watumishi




Katibu wa Afya wa (W)
Ndg Joseph Bura akihakiki vyeti vya watumishi

Monday, August 1, 2016

WILAYA YA  CHEMBA

FAX/SIMU 026 2360175
E-MAIL:dedchemba@yahoo.com
S.L.P 830 CHEMBA
DODOMA.